Filed under: Mashairi
Mpenzi mwandani mahabubu
Naanza kwa kukuomba samahani
Kuandika kwa lugha hii legevu
Nilijaribu lakini sikuweza
Kuyasarifu maneno matamu
Kwa lugha muafaka ya kimapenzi
Mara nyingine ninaahidi
Kutakalamu kwa lugha inayofaa
Bidii nitafanya
Kuyaelewa machungu na matamu yangu
Kwa lugha tukufu isiyo yangu
Badala ya hiki kishairi duni,
Nitakwandikia poem
Nitajitahidi mpenzi
Maneno kuyaelewa
Si kwa jicho la kwangu kijijni
Bali kwa mboni na urazini wa kule kulikotukuka
Nitayatongoza machozi yangu
Kububujika kwa vokali na konsonanti za kimombo
Makali ya moyo wangu kulipuka kwa Kireno,
Kitaliani au Kituruki
Badala ya huu msamiati nilokujazia hapa,
Nitakuwa na vocabulary Mpenzi nitakusifu
Kwa majina ya mimea, wanyama na ndege
Wasiopatikana kwetuNitakutungia koja
Nilirembe kwa vito na maua ya nchi za baridi
Au mimea ya jangwaniNisamehe kwa sasa mpenzi
Naikumbuka tu lugha yangu
Ilonitoa tumboni mwa mama
Ninajua mpenzi
Ni vigumu kwangu kujieleza
Vigumu kwako kuelewa
Nyimbo za nyumbani kwetu kijijini
Ambako tulitembea pamoja tukivikwea vilima
Mikono yetu ikiwa kama sumaku na chuma
Ni vigumu mpenzi
Wewe kuzikumbuka zile harufu
Za mimea iliyotushangilia
Katika sherehe yetu ya mahaba na huba
Samahani mpenzi
Nimeianza barua hii kwa jina lako la kwanza
Wewe kwako ndilo jinalo la kati
Lililotumika kule nyumbani
Kabla ya kuujua mji,
Ugeni na ustaarabu wake.
Nitakuita kwa jina ajualo nyanyako kutamka
Nitajitahidi mpenzi
Kukujua kwa jina lako la mjini, dini na usasa wake
Niwie radhi mpenzi
Nitasema nawe kwa sauti
Wanaokuona na kukusikia laazizi
Wajue asili na usuli wako
Kwa muda wasikunasibishe
Na ungwana wa lugha uliyoizoea
Kwa mishangao waashame
Badala ya salaale
Wamake na kubweka ’gosh’!
Ningelipenda kuahidi kwenda nawe kupata mlo
Lakini natanguliza samahani
Ni haja yangu kukupeleka kula pizza
Lakini nimetafuta jinale katika lugha yangu
Nikakosa kabisa kabisa
Kwa hivyo mpenzi
Samahani zangu zikitangulia
Nakuahidi ugali wa wimbi
Samaki wa kuchemsha
Na mkunde wa kibakuli cha kando
Mpenzi hitari kula mtori
Jasiri pia kuonja makande,
Rojo la mrenda,
Mukimo na muthogoi.
Tutakula pia sageti,
Managu na wenzao.
Tutanyunyiza mafuta
Matamu ya samli,
Kisha tummemene tombo,
Alochomwa kwa makaa.
Jioni tutakaa
Chini ya uso wa mbalamwezi
Tukichoma ndizi,
Viazi na mihogo
Anga zitachanua
Kwa thureya ya nyota
Zikiimba wimbo bora
Wa mapenzi motomoto
Hewani kutafukizwa,
Uturi wa manukato
Ya samadi kavu inayoungua.
Samahani mahabubu,
Ingawa utatamani,
Kifukuza mbu muafaka,
Hii mwandani, haina viletamaradhi.
Sikio letu kichuna,
Tutamwazima bibi,
Babu akiwa mwenzake
Fikira zetu tuwape pia
Kutusafirisha mbali
Watupatie paukwa pakawa
Za miaka hii na iliyokuwa
Samahani mpenzi
Yameniishia maneno
Nimeyatesa macho yako,
Masikio na fikira zako
Misri kukurudisha
Japo kwa muda kidogo
Nikuandikiapo mara nyingine,
Nitakupeleka Zayuni
Kwenye miji mikuu ya utandawazi.
Amadi
2 Comments so far
Leave a comment
Mzee Amad nimeipitia blog yako nimegundua kwamba swahili uliyoitumia ni fasihi sana na bado si amini ka mluya wa kenya anaweza kuandika swahili ya namna hii ,hii ni kitu ya darasani hata watanzania wenzangu wengi hawawezi andika kama wewe,lugha yako imenyooka sana.
Comment by Aziz April 27, 2009 @ 2:34 amAziz Toronto
Hata mie sijaamini,ni changamoto kubwa kwetu si sote haswa wadhamini wa lugha hii tukufu.kutoka kenya mluo
Comment by George March 19, 2010 @ 12:34 am